MICHUANO YA NCBA GOLF SERIES IMERUDI TENA KWA MSIMU WAKE WA 2024

Benki ya NCBA inafurahia kutangaza rasmi kurejea kwa michuano yake maarufu ya NCBA Golf Series, ambayo inatarajiwa kufanyikia katika viwanja vya Gymkhana Golf Club vilivyopo hapa jijini Dar es salaam.


Mashindano ya NCBA Golf Series jijini Dar es Salaam yanakuja ikiwa ni wiki chache baada ya awamu ya kwanza ya mashindano hayo ambayo pia yalihudhuriwa na Waziri wa Sanaa, Utamaduni na Michezo, Damas Ndumbaro kurindima huko jijini Arusha tarehe 29 Julai.

Mashindano ya NCBA Golf Series jijini Dar es Salaam yanatarajiwa kuleta ushindani wa kusisimua zaidi kwa kukusanya pamoja vipaji mbalimbali vya gofu kutoka pande mbalimbali za Dar Es Salaam. Mashindano ya mwaka huu ambayo yatahudhuriwa na viongozi wa kampuni mbalimbali, mashirika yasiyo ya serikali na wadau, mshindi atazawadiwa kiasi cha pesa taslimu pamoja na begi la gofu lenye thamani ya Shilingi milioni 3 za Kitanzania.

Aidha, kwa gharama za waandaaji mshindi atapata nafasi ya kwenda Nairobi kuhudhuria Fainali Kuu ya NCBA Golf Series mwezi Novemba.

Akizungumza kuhusu mashindano hayo, mwakilishi wa NCBA alidokeza kuwa:“Wageni na watakaokuja pale Gymkhana wanapaswa kutarajia mashindano yenye hadhi na kiwango cha kimataifa. Lengo letu siku zote limekuwa ni moja tu: kuinua vipaji vya Watanzania na kukuza mchezo wa gofu. Hivyo basi mashindano ya wikiendi hii bila shaka yataonesha kwa vitendo adhma yetu”

Pia, mashindano ya mwaka huu yatajumuisha programu maalum ya kuitwa Maisha Ni Hesabu Na NCBA, ambayo ina lengo la kutoa elimu ya kifedha kwa wageni watakaokuwepo, elimu ambayo itawasaidia haswa katika usimamizi, matumizi, na uwekezaji wa fedha zao.

Kando na kampeni hiyo, NCBA Golf Series ya mwaka huu pia imekuja na programu maalum ya kutunza mazingira inayoitwa Make Believe, ambayo inaunga mkono juhudi za serikali katika upandaji miti. Washiriki wa NCBA Golf Series kupitia kampeni hii watapata nafasi ya kupanda miti kulingana na idadi ya magoli au ushindi utakaopatikana.




About life goes on

Blogger | Journalist | Entrepreneur | Fashonista Based in Dar es Salaam, Tanzania.

0 comentários :

Post a Comment